Sunday 4 March 2018

BAVICHA wamtaka Mhe. Shonza na Waziri Mwakyembe wampigie magoti Roma Mkatoliki

Baraza la Vijana Chadema (BAVICHA) limemtaka Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo, Mhe. Harrison Mwakyembe na Naibu wake Juliana Shonza kutengua kauli yao ya kumfungia msanii wa muziki wa Bongo Fleva, Roma Mkatoliki kwani hilo sio jukumu lao.
BAVICHA wamesema kuwa jukumu la kufungia kazi za wasanii wa muziki ni la BASATA hivyo wameshangazwa na kitendo cha Mhe. Shonza kuingilia majukumu hayo ambayo kiujumla hakupaswa kutangaza yeye.
“ Serikali hii haioni kwamba kuna kila sababu hali ya uchumi ni ngumu, lakini leo unakuja unamsimamisha msanii asifanye kazi kwa miezi sita. Kwanza sheria haimpi mamlaka waziri, mamalaka hiyo ameitoa wapi Waziri? mamalaka hiyo ipo kwa BASATA sasa kama yeye anaisimamia BASATA aelekeze BASATA wafanye kazi hiyo, sio Naibu Waziri. Kama BARAZA tunaona jambo hili kwamba kiukweli Naibu Waziri Shonza amepotoka, Naibu waziri amekosea tumesikitishwa sana na tuna kila sababu ya kusema na kukemea. Serikali na Waziri mwenye dhamana anapaswa kutengua maamuzi yake na wale waliochelewa nyimbo hizo zikapigwa muda mrefu takribani mwaka mmoja na wenyewe wanapaswa kuchukuliwa hatua, “amesema Mwenyekiti wa BAVICHA, Ole Sosopi jana Machi 03, 2018 kwenye mkutano wake na Waandishi wa Habari.
Kwa upande mwingine BAVICHA wamelitaka Baraza la Sanaa Tanzania kufanya kazi zake kiuweledi bila mashinikizo kutoka kwa watu binafsi.
Alhamisi ya Machi 01, 2018 Serikali kupitia Wizara ya Habari ilitangaza kumfungia msanii wa Muziki wa Bongo Fleva, Roma Mkatoliki kutojihusisha na muziki kwa miezi sita agizo ambalo lilitangazwa na Naibu Waziri wa Wizara hiyo, Mhe. Juliana Shonza.
Soma zaidi kuhusu sababu za Roma Mkatoliki kufungiwa–> Roma Mkatoliki apigwa ‘STOP’ kufanya muziki, Nay wa Mitego apewa onyo kali
Kwa upande mwingine Sosopi amesema kuwa hakuna Mtanzania anayependa kuona maadili ya Watanzania yakivunjwa lakini BASATA watoe hukumu pale panapostahili sio kwa kukaa muda mrefu huku wakisikiliza nyimbo hizo baadae ndio wanakuja kufungia.

No comments:

Post a Comment